Home » Articles » HEALTH

MADHARA YA UVUTAJI WA SIGARA

MADHARA YA UVUTAJI WA SIGARA


Katika moshi wa sigara, zaidi ya kemikali 400 zimegundulika kuw ana madhara makubwa katika afya. Mvutaji mdogo hutumia nusu ya pakiti ya sigara kwa siku na kujikuta akiathiri mwili wake kwa kemikali hizi mara 3500 kwa  mwaka. Hata hivyo, vitu vitatu hatari zaidi katika sigara ni:

1.     Tar: hiki ni kisababisha kansa katika mwili.

2.   Nicotine:   Hiki ni kitu chenye sumu ambacho kwa muda mrefu san akimetumiwa kama dawa ya kuuwa wadudu na sumu ya panya. Inachukua nafasi ya pili kama sumu kali kabisa kwa athari yake mbaya katika mwili wa binadamu.

3.     Carbonmonoxide: Hii ni gesi inayopatikana katika moshi wa sigara.

Madhara mbalimbali ya vitu vinayopatikana katika moshi wa sigara ni kama yafuatayo:

1.    Kuharibika kwa utando mlaini katika njia za hewa: katika njia ambayo pumzi hupita kuna kama tabaka fulani ambalo ni laini limezunguka katika njia. Tabaka hili hufany akazi ya kuzuia vumbi vumbi linaloingia pamoja na hewa. Ile tabia ya uvutaji hufanya vile vitu vinavyopatikana katika moshi wa sigara kuganda katika utando huu na kusababisha njia kuwa nyembamba kwa kule kuongezeka kwa takataka na kemikali katika njia, hivyo kumfanya mvutaji apate shida ya pumzi hapo baadaye.

2.   Vidonda vya tumbo: uvutaji wa sigara huchochea utengenezaji wa acid ambayo huweza kumletea mvutaji huyo vidonda vya tumbo.

3.    Matatizo katika mfumo wa upumuaji:  wavutaji hupata shida katika koo na mapafu hivyo kupata kifua mara kwa mara na maumivu na mwishowe kupata madhara makubwa katika mfumo mzima wa upumuaji kutokana na kuharibika kwa mapafu kama tutakavyozungumzia katika pointi namba 7 hapo chini. Hali ya hewa huwaathiri sana wavutaji sigara kwani hupata pneumonia na asthma.

4.  Udhaifu katika mifupa (Osteoporosis): katika moshi kuna metali ijulikanayo kama cadmium ambayo inaweza kusababisha matatizo katika mifupa, hii husababisha kupoteza asilimia 30 ya calcium katika mifupa. Kwa wanawake uvutaji wa sigara umeonekana kuzuia shughuli ya estrogen na kitu chochote kinachozuia estrogen kufanya kazi husababisha udhaifu katika mifupa (Osteoporosis) na hii huweza kusababisha maumivu ya mara kwa mara katika mifupa.

5.   Kuwahi kumaliza kufikia mzunguko wa mwezi (Menopause): Menopause ni ile hali ya mwanamke kufikia mwisho wa mzunguko wake wa kila mwezi ambao humpelekea kushika ujauzito, hali hii huanza kutokea akifikia umri wa miaka 45 – 55, hutofautiana. wanawake wanaovuta sigara hufikia menopause miaka mitano mapema zaidi ya wasiovuta.

6.   Athari kwa wenye mimba: wanawake wanaovuta sigara huwa katika hatari kubwa sana ya mtoto kutoka kabla ya siku zake (Abortion) au kuua mtoto tumboni. Au hata mtoto kufa mapema zaidi pindi atakapozaliwa.

7.     Kuharibika kwa Alveoli za mapafu (Emphysema):  ile harufu kali ya moshi huharibu alveoli ndogo ndogo katika mapafu. Hii kwa kiasi kikubwa sana hupunguza eneo ambalo Oxygen hukutana na damu na hivyo kusababisha  hali inayoitwa Emphysema. Hali hii hujitengeneza taratibu sana na kimya kwa muda mrefu. Wavutaji wote wana Emphysema kwa kiwango fulani Lakini kutokana na eneo kubwa wanaloishi ambalo hupatikana Oxygen, watu wengi hawajui kwamba wana hali hii. (watu wengi wana takriban alveoli milioni 300 katika mapafu yao) hivyo ni vigumu kugundua hali hii na baadhi hujijua pale wanapofanya mazoezi kwa mfano, na kuhisi ugumu wa pumzi.


8.      Upungufu wa uwezo wa kubeba oxygen katika damu: Carbon Monoxide (CO) inapatikana katika moshi. Uhusiano wa Carbon Monoxide kwa Haemoglobin ni mkubwa mara 200 zaidi ya Oxygen. Hivyo baadhi ya haemoglobin ya damu huzuiwa na Carbon Monoxide kwa wavutaji kwani haemoglobin badala ya kuchukua Oxygen huenda katika Carbon Monoxide na hivyo uwezo wa kubeba oxygen katika damu hupungua.

9.  Kansa/Saratani: Katika asilimia kubwa ya watu wenye kansa hupatikana kutoka kwa wavutaji wa sigara, saratani za ngozi, koo, utumbo, kibofu, mdomo n.k. vilevile saratani ya figo, kongosho, tumbo na kizazi imeonekana mara chache kwa wavutaji wa sigara.

10.Kupungukiwa na vitamin: Uvutaji wa sigara husababisha upungukiwaji wa Vitamin hasahasa Vitamin C. ule uvutaji wa sigara moja tu unaweza kupunguza kiasi cha Vitamin C ambacho kinaweza kulingana na ukubwa wa kutumia chungwa moja tu. Hivyo inashauriwa kula sana Vitamin C ili kurekebisha hali hii.

11. Uvutaji wa sigara unaweza kusababisha kisukari: Nicotine huchochea sukari katika damu kwa kuilazimisha au kuichochea Adrenaline na Non Adrenaline ambayo hufanya ini na misuli kupeleka sukari katika mishipa ya damu. Hii hufanya kongosho ifanye kazi ya kutoa Insuli mara kwa mara ili kudhibiti sukari kama kawaida yake na kutokana na kufanya kazi huku mara kwa mara hufanya kongosho ichoke haraka na kushindwa tena kudhibiti sukari, hivyo humsababishia mtu huyu kisukari.

Kwa upande wangu hizo ndizo athari zinazotokana na uvutaji wa sigara, hivyo basi jaribu kulinganisha yale manufaa ya muda mfupi anayoyapata mvutaji na hasara zake. Hapo utaona kwamba uvutaji wa sigara ni hatari sana kwa afya yako, na ni bora ujitahidi sana uache ili kuboresha afya yako.

 

 

 

 

Category: HEALTH | Added by: Admin (12/Jul/2013) | Author: Yahyou M. Yahya E W
Views: 3134 | Tags: sigara, moyo, madhara, mapafu, damu, uvutaji, afya | Rating: 3.0/2
Total comments: 0
Name *:
Email *:
Code *: