Home » 2017 » December » 25 » SAFARI 7 ZA AJABU ZA SINDUBAD (Part 1)
22:16
SAFARI 7 ZA AJABU ZA SINDUBAD (Part 1)

SINBAD BAHARIA NA SAFARI ZAKE SABA



SEHEMU YA KWANZA

Hindubad mbeba mizigo

KATIKA utawala wa Khalifa Haroun Rashid, aliishi katika jiji la Bagdad maskini aitwaye Hindbad. Siku moja, wakati hali ya hewa ilikuwa ya joto kali, Hindbad alipata tenda ya kubeba mzigo mzito kuupeleka mbali sana kutoka sehemu hiyo ya mji ambako aliishi. 

Alitaabika na joto na uchovu sana, na akiwa bado na safari ndefu ya kwenda, aliingia katika mtaa mmoja ambapo hewa yenye ubaridi mzuri ilipiga juu ya uso wake, na sehemu za kando ya barabara za mtaa huo zilikuwa zikinyunyiziwa na marashi ya waridi.

Alifurahi kupata mahali pa kupumzika kama pale, akaweka mzigo wake, na akaketi kando yake, karibu na nyumba kubwa.
Madirisha ya nyumba hiyo yalikuwa wazi, na Hindbad aliburudishwa na harufu ya manukato ya kitajiri ambayo yalitoka ndani. vilevile alisikia sauti nzuri ya vyombo vya muziki vya aina zote, vikichanganywa na kutoa sauti nzuri zaidi, na nyimbo nzuuri zilizokuwa zikiimbwa na ndege wadogo wadogo waliokuwa maeneo hayo. 

Hindbad hakuwahi kuwa katika sehemu kama ile kabla, na alihisi hamu kubwa ya kujua ni nani mwenyejumba kubwa kama lile na utajiri wote huo na anaeshi kwenye mandhari nzuri sana. alipomuona mtumishi amesimama kwenye lango katika lile jumba zuri, taratibu alijivuta kuelekea kwa huyo mtumishi. Na kwa upole na unyenyekevu, Hindubad akamsalimia yule mtumishi na kuuliza jina la tajiri mwenye jumba hili.

“Inawezekana?” mtumishi aliuliza. “Kwamba wewe ni mgeni sana kiasi ambacho humjui mwenye Jumba hili? Sindubad baharia msafiri maarufu aliyezunguka ulimwengu mzima! Hakuna yeyote katika mji huu asiyemfahamu!”

Masikini Hindubad ambaye siku zote alikuwa akisikia utajiri wa ajabu wa Sindubad baharia, kwa huzuni kubwa kabisa aligeuka nyuma na kurudi kwenye ule mzigo wake mzito, akaugemea na kuanza kulia.

“Kuna tofauti gani kati ya huyu mtu mwenye bahati na mimi?” Aliendelea kulalamika mwenyewe. “Kila siku naishi maisha ya tabu na uchovu, mwili wangu umechoka na ngozi inazeeka kwa umasikini uliokithiri, kazi zote ngumu ninazofanya mwishowe naambulia tu mkate kwaajili ya familia yangu, wakati Sindubad yeye anakula utajiri wake na anaendesha maisha yake kwa raha na urahisi kabisa. Ooh!! Jamani, amefanya nini mpaka ametajirika hivi na mimi nina kosa gani mpaka napata shida hii!!”

Alipomaliza kujisemea hivyo, alijiangusha chini kama mtoto anayetaka kitu fulani, huku akilia na kufuta machozi kwa uchungu wa hali yake ngumu sana ya maisha.

Wakati Hindubad anaendelea kuyaendekeza malalamiko yake na huku akinung’unika, akaja mtumishi mmoja kutoka kwenye lile jumba na kumshika mkono na kumwambia kwamba tajiri Sindubad haraka sana angependa kuzungumza naye.

Hundubad alishtuka sana kusikia hivyo, akajua tu kwamba huenda Sindubad amesikia jinsi alivyokuwa akinung’unika na huenda anamuita ili akamsute au akamuadhibu.

Basi akajaribu kukataa kwa kutoa kisingizio kwamba ana haraka sana na hivyo asingeweza kupata muda wa kuzungumza, pia alisingizia kwamba hawezi kuacha mzigo wa watu pale barabarani kwani huenda ungeibiwa.

Hata hivyo, mtumishi wa Sindubad hakutaka kabisa kusikiliza visingizio hivyo kwani ilikuwa tayari ni amri ya bosi wake, na amri ya bosi wake huwa hairudi nyuma hata kidogo. Kwa kuondoa udhuru huo mtumishi yule aliwaita baadhi ya watumishi wenzake wakae pale nje kwa kuulinda mzigo ule ili Hindubad asipate kisingizio kingine cha kushindwa kuingia ndani kwenda kuonana na Sindubad.

Kisha akampeleka mpaka ndani kwenye holi moja kubwa ambapo kulikuwa na meza kubwa iliyozungukwa na watu waliokaa kama kwenye mkutano fulani hivi. Kwenye meza ile kulikuwa na vyakula vya aina mbalimbali vilivyotengwa kwenye vyombo vya rangi ya dhahabu na fedha.

Mwisho kabisa wa meza ile alikaa bwana mmoja mwenye uso wa heshima mwenye ndevu ndefu nyeupe aitwaye Sindubad! 

Uwoga wa Hindubad ukazidi baada ya kuona watu wengi waliokaa katika meza ile, akaanza kutetemeka na kusitasita kwenda.

Sindubad kwa heshima na upole akamkaribisha Hindubad na kumuomba akae karibu yake. Akaamuru awekewe kiti akae upande wake wa kulia, kisha akampatia chakula na kinywaji.
Wakati Hindubad anakaribia kumaliza chakula, Sindubad akamuuliza kuhusu jina lake na kazi yake.

“Jina langu muheshimiwa naitwa Hindubad,” alijibu Hindubad. “Na sina kazi zaidi ya kubeba mizigo.”

“Vizuri,” alijibu Sindubad.  “Mimi na wenzangu hapa tunayo furaha kukuona; lakini nilituma wakuite kutokana na maneno niliyoyasikia ukitamka wakati nimesimama katika dirisha lile pale.”

“Haaa! Muheshimiwa....” Hindubad alishtuka kusikia hivyo na kusimama ghafla kutoka kwenye kiti alichokuwa amekalia. “Ninakiri bwana, ni hali ya uchovu na joto la mchana huu ndivyo vilinifanya nikose busara na kusema yote hayo, na nakuomba radhi sana nisamehe!”

“Rafiki yangu mpendwa,” alisema Sindubad. “Mimi sio dhalimu kiasi cha kukosewa na wewe, na kinyume chake ni kwamba, nakuonea sana huruma juu ya hali yako. Na nilipoamuru uletwe hapa ni kwasababu nilitaka kukuthibitishia na kukuhakikishia kwamba sijawa katika hali hii ya raha na furaha bila ya kupitia mitihani na vikwazo mbalimbali vigumu sana katika maisha yangu na kukutana na hatari kubwa sana kiasi ambacho mtu hawezi kufikiria wala kuamini. Ndiyo vijana wangu!”

aliendelea kusema huku akiwaangalia watumishi wake waliokuwa wamemzunguka katika meza ile. “Nawahakikishia kwamba, magumu yaliyonikuta yalikuwa ni ya hali ya juu kabisa kiasi ambacho yalitosha kabisa kumkatisha tamaa mtu yeyote kujiingiza katika hatari hiyo kila wakati kwa lengo la kutaka utajiri.”

Aliendelea kuwaambia. “Na kuwathibitishia ukweli wa haya ninayoyasema sasa, kama mtanipa usikivu wenu vizuri, nitawasimulia  mitihani migumu na yenye kusisimua niliyokutana nayo katika safari zangu saba za kutafuta mali na utajiri.”

Wote waliokuwa pale walikubali na walikuwa na hamu kubwa sana ya kutaka kujua nini kilimkuta Sindubad katika hizo safari zake saba.

Sindubad akaamuru mtumishi wake mmoja auchukue mzigo wa Hindubad na aupeleke mahali ambapo unatakiwa ufikishwe na kisha akaanza kuwasimulia juu ya safari yake ya kwanza......

Je kuna nini kwenye safari ya kwanza? Bofya hapa uendelee kusoma....

Category: Stories & Entertainment | Views: 879 | Added by: badshah | Rating: 0.0/0
Total comments: 81 2 »
8 goku  
0 Spam
Nzuri had I naa dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry dry Mme elewa. Au Mme lewalewa happy happy happy

7 goku  
0 Spam

5 alkastar  
0 Spam
Waiting for part 2 admin

6 badshah  
0
Part 2 iko njiani usijali....

4 akidas  
1 Spam
Yah nzuri

3 akidas  
0 Spam
Fantastic

1-5 6-7
Name *:
Email *:
Code *: