Home » 2017 » October » 3 » Alibaba na wezi 40 Part 2
22:39
Alibaba na wezi 40 Part 2

SEHEMU YA PILI

Kutoka sehemu ya kwanza:

Baada ya Alibaba kuingia pangoni na kuona mali zote zile na kujisemea moyoni kuhusu mali zile:

 Kwa kuona wingi wa mali hizi Alibaba alijifikiria moyoni kuwa sio kwa miaka michache tu, hii itakuwa ni karne na karne wezi wanapora mali za watu na kuja kuzificha humu.

 

ENDELEA SEHEMU YA PILI

“Hazina nyingi kiasi gani hiki!!” alisema Alibaba. ‘na sasa nimezipata’ alifikiri kidogo. ‘wezi  hawa hawawezi kukaa na mali yote hii. Lazima nichukue kiasi cha dhahabu nikajiwekee mwenyewe nyumbani.’

Alisema tena yale maneno “Fungukaa sesmiiii” na lango likafunguka, kisha akenda kuwachukua punda wake watatu aliokuwa amewaficha vichakani.

“Leo ninawapa habari njeeema” aliwaambia punda wake. “leo mtabeba dhahabu na sio kuni kama mlivyozoea kila siku. Aliwachukua punda wake mpaka karibu na lile pango na kuwaacha nje kasha yeye akaingia tena ndani. “Punda watatu na makapu sita” Alisema alibaba, “Nitajaza makapu yote haya sita dhahabu”.  Alibaba alichukua makapu yale sita na kujaza kila aina ya dhahabu zilizopo ndani ya lile pango kisha akachukua baadhi ya kuni chache tu kuziweka juu ya kila kapu  ili kuzificha zile dhahabu ndani ya kapu zisionekane na watu akiwa njiani, kisha akatoka na kusimama mbele ya lile pango kwa nje na kusema “Fungaaaa Sesmiii!!!” lile pango likajifunga kwa sauti kubwa, Alibaba alitabasamu na kuondoka kuelekea mjini.

Alibaba hakuelekea sokoni kama kawaida yake siku zote, badala yake aliwaongoza punda wake mpaka nyumbani kwake. Aliwapeleka mpaka kwenye kibanda chao na kufunga mlango, kisha akatoa zile kuni chache alizoweka juu ya kapu na kubakia na kapu zake sita zikiwa zimejaa dhahabu.

Alisubiri mpaka giza lilipoingia. Hakutaka mtu yeyote aone hazina ile. Alizichukua kutoka kwenye banda la punda wake na kuzipeleka mpaka ndani kwake kisha akazimimina zote chini fungu moja. Akamuita mke wake kutoka jikoni.

“Angalia!” alisema Alibaba kwa furaha. “sisi ni matajiri sasa mke wangu!, sitafanya tena kazi ya kukata kuni!,  tutaweza kula vyakula vizuri vizuri sasa na kuvaa mavazi mazuri!”

Mke wa Alibaba alipoziona zile dhahabu,  alishangaa sana. “sijawahi kuona dhahabu nyingi kiasi hiki!” alisema kwa mshangao huku akipepesa macho. ‘lakini Kassim ndiye tajiri, na sio wewe!, umezipata wapi hizi? Au umeziiba? .

Basi Alibaba alimpa stori nzima juu ya wale watu 40 na maajabu ya lile pango na mali zilizopo mle ndani.

“Umeona sasa!” Alisema alibaba “kwahiyo nimeziiba, lakini nimeziiba kutoka kwa wezi hivyo hakuna tatizo lolote. Sasa itakuwa vizuri ukiitunza siri hii, usimwambie mtu yeyote kuhusu hizi dhahabu zetu. “sawa” alijibu mke wake, “itabidi tuchimbe shimo na kuzihifadhi humo, hapo zitakuwa salama. Lakini kabla ya kufanya hivyo itabidi tuzipime ili tujue tuna dhahabu kiasi gani. Nitakwenda kwa  kassim na kumuazima mke wake mizani”.

“Hilo wazo zuri sana” alisema Alibaba, “nenda kaazime hiyo mizani kwa mke wa Kassim wakati mimi huku nachimba shimo”

Mke wa Alibaba alitoka kuelekea kwa Kassim  ambapo ni pembeni kidogo ya mtaa wao. Alifika na kusimama nje ya jumba kubwa la Kassim na kugonga mlango mkubwa wa mbao. Alipokuwa akisubiria kuja kufunguliwa, alisema moyoni huku akitabasamu, “ Sasa mimi na Alibaba tunaweza kununua nyumba kubwa ya kifahari kama hii”.

Mmoja wa watumishi wa Kassim alikuja kumfungulia mlango na kumpeleka mpaka sebuleni alipokuwa amekaa mke wa Kassim.

“Tafadhali, unaweza kuniazima mizani yako?” Alimuomba mke wa kassim “ Nataka kupimia nyama na nitakurudishia baadaye usiku huu huu”

Mke wa Kassim  alikunja uso kwa mshangao. “Alibaba ni masikini” Alijisemea moyoni. “Lakini mke wake anataka kupima nyama. Nyama ni ghali sana. Amepata wapi hela ya kununua nyama huyu?.

“Ndio nitakuazima mizani” mke wa Kassim alisema. “Nitaenda kukuchukulia zipo jikoni”.

Wakati mke wa kassim yupo jikoni, akazishusha zile mizani kutoka kwenye shelfu kisha akachukua asali na kupaka kwenye kitako cha mizani ile. “lazima nijue aina gani ya nyama anayopima, lazima itaganda huku chini ya mizani na nitajua ni nyama ya aina gani” Alijisemea moyoni mke wa kassim huku akielekea sebuleni kumpelekea ile mizani. “hii hapa, unaweza kukaa nayo muda wowote tu unaotaka” Alimpatia mke wa Alibaba. Kisha akaondoka.

Mke wa Alibaba alipofika nyumbani alifanya haraka sana  kupima dhahabu zile na kwa furaha kubwa sana alimkimbilia mumewe kule alipokuwa akichimba shimo.

“Mume wangu!!” alisema mke wa Alibaba, “sisi kwa uhakika ni matajiri kabisaaaaa, tuna dhahabu nyingi sana za kutosha kwaajili ya maisha yetu yote yaliyobaki”.

Alibaba alipiga makofi na kucheka. “Ni furaha iliyoje” Alisema Alibaba, “mtoto wetu Khalid atakuwa tajiri na mwenye furaha pia!, zirudishe hizo mizani haraka, hatutaki Kassim na mkewe wajue siri yetu hii”

Hivyo basi, mke wa Alibaba alichukua zile mizani na kuzirudisha kwa mke wa Kassim. Hakuona dhahabu ambayo ilikuwa imeganda kwenye asali chini ya mizani ile.

“Hii hapa mizani yako” alimpatia mke wa Kassim, “ Nakushukuru sana kwa kuniazima”.

“Karibu sana” mke wa kassim alijibu. “Umeshapima nyama?”

“ooh! Ndio” alijibu mke wa Alibaba, “tena tumepata nyama nyingi”.

Mke wa Alibaba alipoondoka, mke wa Kassim akainua mizani kuangalia chini yake na kuona dhahabu imeganda kwenye ile asali aliyopaka.

“Dhahabu!!!” alisema kwa mshangao mkubwa sana. “Nilijua tu hawa walikuwa na siri!, wamepata wapi hii dhahabu?”

Je nini kitaendelea? Usikose kusoma sehemu ya tatu ya hadithi hii.

 

Category: Stories & Entertainment | Views: 819 | Added by: Admin | Tags: alibaba, wezi | Rating: 2.0/1
Total comments: 4
3 mannor  
-1 Spam
Mke wa kassim kashaniudhi

4 badshah  
0
hahahaha Anaonekana ana roho mbaya

2 don  
0 Spam
Nzuri sana nimewasikilizishia ndugu zangu nyumbani wameipenda sana

1 goku  
0 Spam
Nzuri sana biggrin [color=yellow][hide]

Name *:
Email *:
Code *: